Wednesday, January 23, 2013

Msaada Tutani..

Dada Rose, mimi ni msichana nipo kwenye ndoa zaidi ya miaka mitatu sasa na namshukuru Mungu nimebahatika kupata watoto wawili, kwasababu ya ndoa ilinibidi nibadilishe dini kutoka mkristo na kwenda kuwa muislam kwasababu mume wangu yeye ni wa huko na pia ni mchanganyiko wa kiswahili na kiarabu.

Dada kabla mume wangu hajanioa mimi alishaoa na kuzaa watoto wawili wakike lakini kutokana kutofautiana kwake na mke wake wakaachana na baada ya muda ndio tukakutana na kuoana, lakini dada tokea nimeingia kwenye hii ndoa sina amani yani ni mimi na mume wangu na wanangu tu wakwe zangu hawanipendi mawifi ndio hata hawataki kuniona nashindwa kuelewa eti kisa mtoto wao ameoa mswahili walitaka akaoe muarabu mwenzao.

Kinachonishangaza kwanini wanichukie mimi wakati mimi ni mke wa pili na wakwanza pia alikuwa mswahili tena ndio mashoga kabisa na mama mkwe wangu watu wa pembeni wanaowajuwa wananihadithia yani wanapika na kupakuwa kwa jinsi wanavyopendana, imefikia sasa mama mkwe hakanyagi kabisa kwangu, hana muda hata kujulia wajukuu zake hali na mbaya zaidi sasa hivi kamsusa hadi mtoto wake haongei naye kila mwanaye anapompigia simu yule mama anakata na akienda nyumbani hataki kabisa kuongea naye na anamwambia itabaki kuwa hivyo mpaka aniache.

Kuna kipindi dada mume wangu aliumwa sana akalazwa Agakhan yani aliumwa nikajuwa sasa anakata roho yani kila ndugu yake ninaye mpigia wananijibu majibu ya ajabu mpaka kaka yake mmoja akaniambia hana muda wa kuja kumuona, nililia sana mpaka anapona ni ndugu zangu, wazazi wangu na rafiki wa mume wangu ndio waliokuja kumuona na kunipa moyo. Sikuamini kama kuna watu wa katiki hivyo kwa ndugu yao kisa chaguo la moyo wake.

Kwa ninavyomjuwa mume wangu naamini ananipenda, na ananihudumia vizuri sana kila ninachotaka ananipa nakaa mahali pazuri naendesha gari nzuri yani ukiacha hizo kero za wakwe na mawifi namshukuru Mungu maisha ni mazuri tu, yaani sasa hivi nimechoka nimeamua na mimi sasa sitaki kujipendekeza kwao tena nitakaa tu kimya nifwate ndoa yangu na kumtunza mume wangu hao wakinipenda wasinipende shauri yao maana nimeshaumiza sana kichwa.

Natumaini nitafanya jambo la maana na kama sio naombeni pia mnishauri maana sina la kufanya.

4 comments:

  1. Umeamua la maana.Achana na hawa ndugu wa mume.Kama walisita kuja kumjulia hali ndugu yao ,unategemea nini kut8ka hawa watu? hata huyo mumeo pia awe na msimamo kama wa kwako.Ndio kuna radhi ya mama lakini hata mungu matendo kama haya ya familia ya bwana HAYAPENDI.Wewe endelea na kumtunza mumeo na Mungu atakubariki.

    ReplyDelete
  2. Umeamua uamuzi mzuri sana hao ndugu hua hawaridhiki hata uwafanye nini wewe angalia mume wako na ndoa yako tu achana naowakujuliehali wasikujulie hali hiyo ni juu yao kama ndugu yao ameumwa waneshindwa kuja kumuona unafikiri we ndo watakujali. Songa mbele vikwazo ni vingi kwenye maisha ila tu kubwa usiache kumuomba mungu wako ndio kinga kubwa katika maisha. Pole sana dada yataisha tu

    ReplyDelete
  3. tena uamke sasa maana hatuombei kifo ila km mwny Mungu atamchukua wakwanza watakufukuza baada ya eda tu bila mali yoyote..mwambie akushirikishe kwenye vitu atakavonunua au anavomiliki.km jina muansike yakwenu au 1 ya wanao..wakee na mawifi washakuonesha dalili mapemaaaaa.changamka.
    salha.

    ReplyDelete
  4. mh dada umenitisha na stori yako maana na mimi nina mchumba wa kiarabu tena muarabu pure hana tone hata la uswahili sasa mswahili mimi nikija kuolewa si ndo ntateseka kabsa kama huyo wako alikuwa chotara inamaana ana uswahili ndani yake lakini wakasahau hilo!mh hawa watu wanaoitwa wahindi na waaarabu sio watu wa kuunganisha nao udugu. waelewa wazungu tu.

    ReplyDelete