Monday, September 23, 2013

Hatareee

 BINTI wa miaka 16, Husna amefungukia ndoa yake na mwanaume anayetajwa kwa jina la Juma na kudai anafurahia ndoa yake, Risasi Jumamosi lina mkanda mzima.
Akizungumza na waandishi wetu, Mbande nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam, Husna alisema aliolewa na mwanaume huyo Julai mwaka huu, mkoani Lindi na mwezi uliopita walihamia Dar.

Alipohojiwa kwa nini alikubali kuolewa akiwa na umri mdogo, alisema kwamba alikosa kazi ya kufanya.
Binti huyo aliwashangaza waandishi na polisi pale alipodai kwamba yeye si mtoto mdogo kwani ana mdogo wake mwenye umri wa miaka 15 ambaye ameolewa na amezaa mtoto hivyo yeye asikodolewe macho.
“Mbona mdogo wangu ana miaka 15 ameolewa. Mimi siyo mtoto mdogo ninaijua raha ya ndoa yangu,” alisema Husna.
Waandishi wetu walipotaka kujua kama huwa anapatwa na maumivu anapokutana na mumewe,  alisema anajisikia kawaida kwani alianza mapenzi tangu akiwa shuleni. 
Kama vile haitoshi, binti huyo alisema kuwa huwa anawashangaa hata polisi ambao wanajaribu kulifuatilia suala hilo.
Hata hivyo, Husna alisema kuwa angependa kuendelezwa kimasomo kama akipatikana mfadhili na kuachana na mumewe huyo.
“Nipo tayari kuachana na mume wangu na kwenda kusoma kwa kuwa umasikini ndiyo uliochangia kuolewa mapema,” alisema.
Awali waandishi wetu walipewa taarifa za kuwepo mwanaume aliyeoa mtoto mdogo na majirani wa wanandoa hao na kuwataka kulivalia njuga suala hilo.

”Tunashangaa mwanaume amemuoa binti mdogo sana yaani sawa na mwanaye kabisa. Muda mwingi binti anachezea michanga na watoto wengine. Sijui kamtoa wapi?” alisema mmoja wa majirani hao.
Baada ya kufanyia uchunguzi jambo hilo. Waandishi wetu walibaini nyumba wanayoishi wanandoa hao, ndipo Septemba 14 mwaka huu, waandishi wetu walivamia nyumba hiyo wakiwa na askari ili kumtia nguvuni mwanaume huyo ambaye kwa mujibu wa majirani aliambiwa na watu wake wa karibu na kutoroka eneo hilo.
Akizungumza na waandishi wetu kuhusiana na tukio hilo, Mwakilishi wa Mtandao wa Wanawake Kanda ya Kipolisi Temeke, Eva Michael alisema kuwa wazazi wengi wenye mabinti wadogo hawajui sheria zinazowahusu kama ilivyo kwa Husna ambaye anaona kuolewa katika umri wake ni jambo sahihi kwake.
“Kwa mujibu wa sheria ya ndoa ya mwaka 2009 hairuhusiwi mwanamke kuolewa chini ya miaka 18, kwani huo ni kama ubakaji. Watu bado wanaitambua sheria ya mwaka 1971 inayoruhusu mwanamke kuolewa kuanzia umri wa miaka 14, sheria ambayo imeshabadilishwa, kwa hiyo mume wa Husna anachukuliwa kama mbakaji,” alisema mwanaharakati huyo.
Akibainisha jinsi ya kushughulikia suala la Husna, Bi. Eva alisema kuwa atashirikiana na watu wa Ustawi wa Jamii watakaomjenga kisaikolojia na kumpa hifadhi ya muda kabla ya kuwapata wafadhili watakaojitolea kumsaidia.
Mume wa Husna bado anatafutwa na polisi na amefunguliwa kesi katika Kituo cha Polisi Mbagala Kizuiani yenye  namba, MBL/RB/9435/13 KUBAKA.

Imetoka: Global Publishers

1 comments:

  1. Majibu ya huyo binti yamenihuzunisha sana.ila kama atapatikana mfadhili basi arudi shule

    ReplyDelete